Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, endapo utawala wa Kizayuni wa Israel utaishambulia kijeshi Iran basi utajuta kwa hatua yake hiyo kwani jibu la Tehran kwa uchokozi huo litakuwa kali. Rais Ahmadinejad amebainisha kwamba, anaioinya Israel isithubutu kuanzisha chokochoko ya aina yoyote ile dhidi ya taifa hili; kwani itajuta kwa hatua yake hiyo. Dakta Ahmadinejad amesema, Iran inakaribisha mno kuundwa nchi huru ya Palestina na kwamba, hatua hiyo inapaswa kuwa utangulizi wa kukombolewa ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni maghasibu. Rais wa Iran ameongeza kwamba, madola ya eneo hili la Mashariki ya Kati hayapaswi kuruhusu madola ya Magharibi yaje na kuwa na satwa na udhibiti na kwamba, Iran inawataka wananchi wa eneo hili kuwa macho na kutoukubali uingiliaji wa kigeni katika masuala yao ya ndani. Kuhusiana na suala la Quds, Rais Ahmadinejad amesema, suala hili sio suala la Iran au la nchi za Kiarabu tu, bali kadhia ya Quds ni kadhia ya ulimwengu mzima wa Kiislamu.